Liverpool imekamilisha rasmi usajili wa beki wa kati Jérémy Jacquet kutoka Stade Rennais kwa mkataba wa muda mrefu, huku dili hilo likitajwa kuwa na thamani ya pauni milioni 55 pamoja na pauni milioni tano za nyongeza kulingana na mafanikio ya mchezaji na klabu.
Usajili huo umeanza kutumika rasmi Julai 1, ingawa bado unasubiri kukamilika kwa taratibu za kibali cha kazi na uidhinishaji wa kimataifa. Jacquet, mwenye umri wa miaka 20 na urefu wa mita 1.90, anatajwa kuwa mmoja wa mabeki chipukizi wenye uwezo mkubwa barani Ulaya kutokana na uimara wake wa kujihami, uwezo wa kucheza mipira ya juu na utulivu akiwa na mpira.
Liverpool inaamini Jacquet ataongeza ushindani katika safu ya ulinzi kwa kushirikiana na Virgil van Dijk katika kuimarisha ngome ya mabingwa hao wa England.
Hata hivyo, beki huyo anajiunga na Liverpool akiwa katika hatua za mwisho za kupona jeraha la bega alilolipata mwishoni mwa msimu uliopita akiwa Rennes. Klabu hiyo ina matumaini kuwa atakuwa fiti kwa wakati ili kushiriki maandalizi ya msimu mpya, huku usajili wake ukija baada ya Liverpool kushindwa kufanikisha dili la Marc Guéhi katika dirisha lililopita.



