Baada ya kumalizika kwa msimu wa Ligi Kuu ya NBC, uongozi wa Simba umeelekeza nguvu zote kwenye mchezo wa fainali ya Kombe la CRDB, ukilenga kumaliza msimu kwa kutwaa taji hilo.
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ali, amesema wachezaji, benchi la ufundi na viongozi wote wamejipanga kuhakikisha wanaleta furaha kwa mashabiki kwa kushinda fainali dhidi ya Azam FC.
Mchezo huo wa fainali unatarajiwa kuchezwa Jumamosi, Julai 4, katika Uwanja wa Gombani, Pemba, kuanzia saa 11:00 jioni.
Akizungumza baada ya Simba kuifunga KMC bao 1-0 katika mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu, Ahmed alisema licha ya timu hiyo kuonyesha kiwango bora msimu mzima, walishindwa kutwaa ubingwa kutokana na kile alichodai kuwa ni makosa ya kibinadamu ya waamuzi.
Ahmed alisema mashabiki wa Simba wanafahamu timu yao ilifanya kila lililowezekana katika mbio za ubingwa, hivyo sasa macho yote yanaelekezwa kwenye Kombe la CRDB ili kufuta majonzi ya kukosa taji la ligi.
"Wachezaji tumeshawaambia, ubingwa wa Ligi Kuu tumeukosa kwa mara ya tano. Safari hii hatuhesabii sana kwa sababu kulikuwa na makandokando mengi."
Aliendelea kusisitiza kuwa hakuna nafasi ya visingizio katika fainali hiyo, akiwataka wachezaji kupambana kwa nguvu zote kwa ajili ya nembo ya Simba na furaha ya mashabiki.
"Ubingwa wa CRDB tunakwenda huku hatuna cha kujitetea. Twendeni tukapambane, twendeni tukaipiganie nembo ya Simba na furaha ya Wanasimba."
Ahmed aliongeza kuwa mashabiki tayari wameonyesha imani kubwa kwa timu kutokana na kiwango ilichoonyesha msimu huu, jambo linalowapa wachezaji hamasa ya kupambana hadi dakika ya mwisho.
"Wachezaji wetu wamelielewa hilo. Wako tayari kufa uwanjani kwa ajili ya kuipigania furaha ya Wanasimba. Kila mmoja anafahamu jukumu lililopo mbele yetu ni kwenda kuleta taji la CRDB."
Simba sasa inaingia kwenye fainali hiyo ikiwa na dhamira ya kumaliza msimu kwa taji, huku ikiamini ushindi dhidi ya Azam FC utakuwa zawadi bora kwa mashabiki walioendelea kuiunga mkono katika kipindi chote cha msimu.



