Klabu ya Simba imekanusha taarifa zinazozagaa mitandaoni kwamba baadhi ya mastaa wake wapo kwenye hatua za mwisho kuondoka katika kikosi hicho wakati huu wa dirisha la usajili.
Miongoni mwa wachezaji wanaotajwa kuondoka ni kiungo mshambuliaji raia wa Senegal, Libasse Gueye, ambaye amekuwa sehemu muhimu ya kikosi cha Wekundu wa Msimbazi katika msimu uliopita.
Akizungumza na wanahabari mapema leo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, amepinga vikali taarifa hizo na kusema hazina ukweli wowote. Amesisitiza kuwa Gueye bado ana mkataba na klabu hiyo na ni sehemu ya mipango ya timu kuelekea msimu mpya wa mashindano.
Ahmed amesema kuwa pamoja na Libasse, wachezaji wengine wanaotajwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa wanaondoka, wataendelea kuwa sehemu ya kikosi cha Simba katika msimu ujao.
"Kumekuwa na maneno mengi kwamba Libasse anauzwa, Oura anauzwa au Loemba anaondoka, lakini nikiwa hapa nikiwa nimevaa suti ya bei ghali nawatangazia kwamba hakuna mchezaji hata mmoja ambaye anaondoka. Yoyote bora ambaye unamfahamu bado ataendelea kuwepo na leo kuna habari njema ya Selemani Mwalimu kuendelea kusalia Simba Sports Club," alisema Ahmed.
Kauli hiyo imekuja wakati ambapo mashabiki wa Simba wamekuwa wakifuatilia kwa karibu mabadiliko yanayoendelea ndani ya kikosi hicho kuelekea msimu mpya, huku tetesi mbalimbali za usajili na kuondoka kwa wachezaji zikiwa zimekuwa zikienea kwa kasi.
Aidha, Ahmed Ally amesema Simba bado haijamaliza mipango yake ya usajili na kwamba uongozi unaendelea kufanya kazi kuhakikisha unapata wachezaji wenye uwezo mkubwa na kiu ya ushindani.
"Uongozi umejipanga vizuri kusajili wachezaji wenye uwezo mkubwa na kiu ya kupambana, watakaohakikisha klabu hiyo inarudi kwenye ubora wake na kufanya vizuri katika mashindano yote ya ndani na yale ya kimataifa," aliongeza Ahmed.
Hadi sasa, Simba imekamilisha usajili wa wachezaji kadhaa kwa ajili ya msimu mpya, akiwemo beki Nathaniel Chilambo kutoka Azam FC, kiungo Kelvin Nashon aliyekuwa Pamba Jiji, pamoja na kiungo mshambuliaji Bakari Msimu kutoka Coastal Union ya Tanga.