Kocha Msaidizi wa Simba, Suleiman Matola, amesema kikosi hicho kimefanya maandalizi ya kutosha kuelekea mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania dhidi ya Coastal Union utakaopigwa kesho Alhamisi katika Uwanja wa Isamuhyo.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari kuelekea mchezo huo, Matola amekiri kuwa wanatarajia kukutana na upinzani mkali kutoka kwa Coastal Union, akisisitiza kuwa michezo kati ya timu hizo imekuwa na ushindani mkubwa.
Matola amesema licha ya Coastal Union kutokuwa na matokeo mazuri katika michezo yake ya hivi karibuni, kiwango cha uchezaji cha timu hiyo kinawafanya Simba kutarajia mchezo mgumu.
“Maandalizi yetu yanakwenda vizuri, nina imani haitakuwa mechi rahisi. Simba na Coastal Union ni timu zenye upinzani mkali kila zinapokutana.”
Ameongeza:
“Ukiwaangalia Coastal Union wamekuwa hawana matokeo mazuri lakini wamekuwa wakicheza vizuri na kuonyesha ushindani mkubwa. Hii inatufanya tuamini tutakuwa na mechi ngumu kesho.”
Hata hivyo, Matola amesema Simba imejipanga kuhakikisha inapata alama zote tatu katika mchezo huo.
“Lakini pamoja na ugumu wao, sisi tumejiandaa vyema kuhakikisha tunapata alama tatu katika mchezo wa kesho,” alisema Matola.
Matola azungumzia FVS na kadi nyekundu
Mbali na maandalizi ya mchezo huo, Matola pia amezungumzia matumizi ya FVS katika Ligi Kuu msimu huu, akieleza kuwa teknolojia hiyo imekuwa na umuhimu katika kuongeza usahihi wa maamuzi ya waamuzi.
Kocha huyo amesema Simba imechukua hatua mbalimbali katika mazoezi ili kuwajengea wachezaji umakini zaidi na kuepuka makosa yanayoweza kusababisha adhabu zaidi.
“Ni uamuzi muhimu kuleta FVS kwenye ligi yetu. Tumefanya kazi kubwa uwanja wa mazoezi ili kuongeza umakini kwa wachezaji na kuweza kuepuka yale ambayo yalikuwa hayaonekani na sasa yanaonekana,” alisema Matola.



