Kocha wa Tunisia, Nasreddine Nabi, ameondoka rasmi katika klabu ya Raja Casablanca ya Morocco baada ya wiki kadhaa za mvutano na Mkurugenzi wa Michezo wa klabu hiyo, Rogério Matias.
Mvutano huo ulihusishwa zaidi na sera za usajili, huku Nabi akidaiwa kutoridhishwa na baadhi ya wachezaji waliosajiliwa na klabu badala ya wale aliowahitaji. Pia kulikuwa na tofauti kuhusu mustakabali wa Badr Benoun, ambaye Nabi alitaka abaki katika kikosi lakini uongozi ulikuwa na mtazamo tofauti.
Nabi kupitia ujumbe wake kwenye mitandao ya kijamii amesema hakuwa na nia ya kuzua mgogoro, akisisitiza kuwa hakuna mchezaji, kocha au mtu binafsi aliye juu ya taasisi. Pia amewashukuru mashabiki wa Raja, akiwemo Ultra Eagles na Green Boys, kwa mapokezi na sapoti waliyompa wakati akiwa klabuni hapo.
Kuondoka kwa Nabi kunaongeza sura nyingine katika mabadiliko ya benchi la ufundi la Raja Casablanca, ikiwa ni kocha wa nane kuondoka tangu klabu hiyo imalize msimu bila taji chini ya Josef Zinnbauer mwaka 2024.



