Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, ameanza ziara maalum nchini Hispania kwa ajili ya kufanya mazungumzo na uongozi wa klabu ya FC Barcelona, akilenga kujadili fursa za ushirikiano katika maendeleo ya soka nchini Tanzania.
Mazungumzo hayo yanahusisha maeneo mbalimbali ya maendeleo ya soka, ikiwemo ukuaji wa vipaji, maendeleo ya kiufundi, uendeshaji wa timu za taifa pamoja na kujifunza uzoefu wa Barcelona katika maandalizi ya mashindano makubwa ya soka. Tanzania ni miongoni mwa wenyeji wa AFCON 2027 pamoja na Kenya na Uganda.
Katika ziara hiyo, Makonda anaambatana na wataalamu kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) pamoja na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), huku akitarajiwa pia kushuhudia mchezo wa Barcelona dhidi ya Racing Santander uliopangwa kufanyika Septemba 16, 2026.
Ziara hiyo inalenga pia kufungua fursa za kujifunza na kushirikiana na moja ya klabu kubwa duniani katika maeneo ambayo yanaweza kuchangia maendeleo ya soka la Tanzania, hususan katika malezi ya vipaji, utaalamu wa kiufundi na uendeshaji wa soka.